Thursday, March 1, 2012

KAMPENI YA KUPUNGUZA UMRI WA URAIS HAINA UHUSIANO NA MIMI KUTAKA KUGOMBEA URAIS 2015 – ZITTO KABWE.


 Mambo ambayo Mh. Zitto aliyatolea ufafanuzi,
  1. "Baadhi ya vyombo vya habari vimehusisha kauli yangu ya kutaka kupunguza umri wa kugombea urais na mimi ‘kuutaka urais’. Mimi nikiwa mwanachama na kiongozi wa chama chama changu cha CHADEMA naelewa na kuziheshimu taratibu na kanuni tulizojiwekea za kuomba nafasi mbalimbali za uongozi, ikiwemo nafasi ya urais. Nafasi ya uongozi ndani ya CHADEMA haiombwi kwenye warsha. Iwapo chama changu, wakati muafaka ukifika na kutokana na matakwa ya jamii, kikiona nipewe jukumu lolote sitasita kutekeleza wajibu huo niwe au nisiwe mgombea.
  2. Kwa hivyo, nilichozungumza jana ni kutoa maoni yangu kwamba muda umefika kwa Taifa letu kupunguza umri wa kugombea urais. Maoni yangu haya yanatokana na ukweli kwamba hakuna sababu zozote za kisayansi zinazomfanya mtu aliye chini ya umri wa miaka 40 akose sifa za kuwa Rais. Msimamo huu nimekuwa nao tangu zamani nikisoma shule na haujawahi kubadilika. Hakuna mahala popote katika maoni yangu niliyotoa jana niliposema kwamba nataka umri wa urais upunguzwe ili nipate fursa ya kugombea nafasi ya urais. Pia siwezi kutaka katiba iandikwe kwa ajili yangu. Vilevile kamwe isionekane kwamba matakwa ya muda mrefu ya vijana ya kutaka umri wa kugombea Urais kupunguzwa yanalenga kunipa fursa mimi kwani mimi ni binaadamu naweza nisiwe na sifa za kuwa Rais lakini kukawa na vijana wengine wengi wenye umri chini ya miaka 40 wenye Uwezo na Uzalendo wa kutosha kushika usukani wa nchi yetu. Ni maoni yangu kwamba tupate mabadiliko ya vizazi katika uongozi wa nchi yetu ili kukabili changamoto za sasa zinazokabili Taifa letu.
  3. Tunapojiandaa kutoa maoni kuhusu Katiba Mpya ni vizuri vyombo vya habari vikajikita kutoa taarifa bila kuweka tafsiri au kuwatafasiria maoni ambayo wananchi na viongozi watakuwa wanayatoa kuhusu maudhui ya Katiba Mpya."

0 comments:

Post a Comment